Hadithi za Marudio Jumapili, tarehe 18 Mfungo Sita, 1446, sawa na 22 Septemba 2024.
KUHUSU KUWA NA MATUMAINI NA MWENYEZI MUNGU
SEHEMU YA TANO.
51- Mlango wa Matumaini
Amesema Mwenyezi Munguسبحانه وتعالي :-
5. Na rehema Yangu imeenea (imefunika) kila kitu (Al-A‘raaf, 7:156)
430. Imepokewa kutoka kwa ‘Abdullah bin ‘Amr bin al-‘Asرضي الله عنهما akisema: Alisoma Mtume ﷺ maneno ya Mwenyezi Mungu, yenye kusimulia dua ya Nabii Ibrahim عليه السلام Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hayo yamewapoteza watu wengi. Basi aliye nifuata mimi huyo ni wangu, na aliye niasi, hakika Wewe ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu (Ibrahim:36) na maneno ya Mwenyezi Mungu, yenye kusimulia dua ya Nabii ‘Isa عليه السلام : Ukiwaadhibu basi wao ni waja Wako, na ukiwasamehe basi hakika Wewe ni Mwenye nguvu, Mwenye hekima (Al-Ma’ida, 5:118) alipomaliza kusoma, aliinua mikono yake juu na kusema:
“Ewe Mola wangu! Umma wangu, Umma wangu!” kisha akalia!
Mwenyezi Mungu akamtuma Jibril na kumuagiza kwa kumwambia: “Jibril! Nenda kwa Muhammad ukamuulize–na Mola wako Anajua zaidi- kinamliza nini?”
Basi Jibril akamuendea na kumuuliza. Na Mjumbe wa Mwenyezi Mungu akamjibu – na Mwenyezi Mungu Anakijua- kile alichokisema. Basi Mwenyezi Mungu akamwambia Jibril:
“Ewe Jibril! Nenda kwa Muhammad na mwambie: “Tutakuridhisha kwa Umma wako na wala Hatutakuhuzunisha!” Ameipokea Muslim.
431. Imepokewa kutoka kwa Mu’aadh bin Jabal رضي الله عنه akisema: Alinipakia Mtume ﷺ juu ya punda wake, akaniita kwa kusema:
“Ewe Mu‘adh! Unajua nini haki ya Mwenyezi Mungu juu ya waja Wake? Na nini haki ya waja wa Mwenyezi Mungu, kwa Mola wao?” Nikajibu: “Mwnyezi Mungu na Mutme Wake ndio wanao jua zaidi.” Akasema:
“Haki ya Allah kwa waja wake ni kumuabudu Yeye peke Yake, pasi na kumshirikisha na chochote. Na haki ya waja kwa Mwenyezi Mungu ni kutomuadhibu yeyote yule ambaye hamshirikishi na kitu chochote!”
Nikasema: Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Je, unaniruhusu niwabashirie watu habari hiyo!” Akasema: “Hapana, usiwabashirie; watabweteka!” Muttafaq ‘alayhi. [Angalia pia Hadithi Nam.420, mlango huu huu]
432. Imepokewa kutoka kwa al-Bara’ bin ‘Azibرضي الله عنهما akisema: Amesema Mtume ﷺ : “Mwislamu ataposailiwa [hojiwa] kaburini, atajibu kuwa anashuhudia kwamba hapana mola wa kuabudiwa kwa kweli ila Allah na Muhammad ni Mjumbe wa Mwenyezi Mungu, na hiyo ndiyo maana ya Maneno ya Mwenyezi Mungu: Mwenyzi Mungu Huwathibitisha [huwawezesha] wenye kuamini kwa kauli sahihi, katika maisha ya dunia na ya Akhera (Ibrahim: 27) Muttafaq ‘alayhi.
433. Imepokewa kutoka kwa Anas رضي الله عنه akisema: Amesema Mtume ﷺ : “Pale kafiri anapofanya jambo moja jema basi hulipwa, kwa jema hilo, malipo ya kidunia [hapa hapa duniani]. Lakini mwenye kuamini, huekezewa katika amali zake njema Siku ya Akhera, na hupewa riziki duniani, kwa utiifu wake.”
Riwaya nyengine, ya Muslim, inasema: “Mwenyezi Mungu Hamdhulumu (Hamnyimi) – mwenye kuamini- jema lolote lile alifanyalo; maana hulipwa kwa riziki duniani, na Akhera hulipwa kwa thawabu. Ama kafiri, yeye hulipwa riziki, duniani, kwa mema anayofanya kwa ajili ya Mwenyezi Mungu, lakini akifika Akhera hana kitu chema cha kulipwa.” Ameipokea Muslim.
UFAFANUZI
Bado tumo katika mlango wa kutokata tamaa na umuhimu wa kuwa na Matumaini mema kwa Mwenyezi Mungu, ilimradi Matumaini mema hayo yatokane na Imani thabiti, na yafuatiwe na kuomba msamaha kwa wingi, na kutubu kwa kauli na vitendo. Kutumaini Rehema za Mwenyezi Mungu pasi na kumuamini ni sawa na kutaraji kunywa maji kutoka kwenye jiwe manga (sulubu\gumu) Au kutaraji kupata gudulia la maji baridi Motoni!
Hivyo, Imani, Istighfaar na Tawba, kwa kauli na vitendo ndio chanzo na ufunguo wa kutokata tamaa. Bali ndio shahada ya kupata Radhi za Mwenyezi Mungu سبحانه وتعالى ; maana Imani ni Kauli na Vitendo. Kama ilivyo Ukafiri ni kauli na vitendo.
YALIYOMO NA YATOKANAYO
1. Mwenye kumuamini Allah na Mtume Wake, kamwe hakati tamaa na Mwenyezi Mungu.
2. Shafaa=maombezi ya Mtumeﷺ , Siku ya Kiyama, yanamjumuisha kila aliyemuamini na kumfuata.
3. Hadithi hii, ni miongoni mwa Dalili kubwa, za kuweko Shafaa ya Mtume ﷺ Siku ya Kiyama, kwa waliomuamini na kumfuata.
4. Ukubwa na Wingi wa huruma za Mtume ﷺ kwa umma wake.
5. Ukubwa na Wingi wa Mapenzi ya Mwenyezi Mungu kwa Mtume Wake, Muhammad ﷺ
6. Ikiwa Mtume wa Mwenyezi Mungu anapendwa Naye kiasi hicho, iweje sisi tusiweze kumpenda na kumtukuza anavyostahiki kupendwa na kutukuzwa!
7. Kumpenda Mtume ﷺ ni WAJIBU juu yetu, na ni budi kumpenda zaidi ya kiumbe yeyote mwengine, zaidi kuliko mali zetu, watoto wetu, bali hata nafsi zetu:- لايؤمن عبد حتى أكون أحب إليه من ولده ووالده والناس أجمعين (رواه مسلم -44 – وغيره)
8. Kumuabudu Mwenyezi Mungu, Pekee, pasi na kumshirikisha na chochote kile ni WAJIBU MTAKATIFU wa kila mja, na atayefanya hivyo kwa dhati ni budi kuingia Peponi.
9. Mwenyezi Mungu Ametoa dhamana – kutokana na Fadhila Zake na Ukarimu Wake- kutomuingiza Motoni, yeyote yule atayetimiza WAJIBU wake MTAKATIFU wa kumuabudu, Pekee, pasi na kumsirikisha na chochote kile.
10. Kuhakikishiwa Matumaini mema hakumaanishi ubweteke tu; kwani kila mtu hufanyiwa wepesi kutenda liliyomo katika masjala yake, isipokuwa akiomba asaidiwe. لايرد القضاء إلا الدعاء Ni Dua pekee ndiyo inayoweza kubadilisha au kufuta yaliyoandikwa kwenye masjala.
11. Hatari ya kumsirikisha Allah na kitu chochote kile, iwe katika kumuabudu, katika Majina Yake, Sifa Zake, kutii Amri Zake, na kadhalika: مخلصين له الدين = kwa Kumtakasia Ibada kikamilifu. HAKUNA MCHEZO KATIKA HILI!
12. Kusailiwa kaburini, mara, tu, baada ya kuzikwa, ni Haki. Na hakuna mtu atayeweza kubadilisha, au kubadilishiwa majibu yake, isipokuwa amali zake alizozitenda Duniani.
13. Ni Mwenyezi Mungu, pekee, ndiye Mwenye kumpa Kauli Thaabit, kaburini, yule aliyemuamini; na SI تلقين :IMLA(dictation) ya walio hai! Na hiyo ndiyo maana ya Aya ya 27 ya Surat Ibrahim.
14. Umuhimu wa kumuombea maiti, kwa Mwenyezi Mungu, Ampe kauli thabit, na SI UFIDHULI wa kumfundisha aseme nini! Munkar!
15. Ni amali za mja, alizotenda duniani, ndizo zitazomsaidia au kumtosa baada ya kufa.
16. Maiti anaombewa haombwi! Akiombwa ameshirikishwa na Mwenyezi Mungu!
17. Hakuna amali isiyo na malipo kutoka kwa Mwenyezi Mungu! Wema kwa wema na uovu kwa uovu.
18. Wema wa kafiri duniani hulipwa hapa hapa duniani; akienda Akhera hana lake ila amali za ukafiri wake.
19. Ukafiri unafuta malipo ya amali njema Akhera.
20. Wema wa Muumini hulipwa duniani na Akhera, au huekezewa ili alipwe vyema zaidi Akhera. Duniani hurahisishiwa rizki yake kwa utiifu wake.
21. Imani haifuti, bali inaweza kuchelewesha tu, malipo mema, hapa duniani, lakini ni budi kulipwa mema, Akhera.
22. Kipimo na Kigezo cha kukubaliwa au kukataliwa Amali za Mwanadamu ni Imani sahihi na utakaso wa Nia.
23. Ewe Mwenye kuamini! Usikate tamaa kutokana na Rehema za Allah!
وبالله التوفيق
الحقيرإلى الله تعالى عبد القادر شريف آل الشيخ أبى بكربن سالم
INAENDELEA…
Imetayarishwa na Sayyid Abdulqadir Shareef
Kutoka Kitabu cha: Kitalu cha Waja Wema: Maneno ya Muokozi wa Umma, ambacho ni tafisri kamili ya رياض الصالحين من كلام سيد المرسلين للإ مام النووي kilicho tungwa na Imam al-Nawawi na kufasiriwa kwa Kiswahili na Sayyid Abdulqadir Shareef.
NI RUHUSA KUNUKUU NA kuweka kwenye FB yako au kwenye Whatsup na kwenye Makundi ya Mitandao ya Kijamii za Kiislamu, kwa lengo la kusambaza na kuelimisha Dini. Changia kusambaza Dini, ujipatie thawabu.
kcwajawema@gmail.com
Leave a Reply