Hadithi za Marudio Jumapili, tarehe 25 Mfungo Sita, 1446, sawa na 29 Septemba 2024.
KUHUSU KUWA NA MATUMAINI NA MWENYEI MUNGU
SEHEMU YA NANE NA YA MWISHO.
51- Mlango wa Matumaini
Amesema Mwenyezi Munguسبحانه وتعالي :-
Na rehema Yangu imeenea (imefunika) kila kitu (al-A’raaf: 156)
443. Imepokewa kutoka kwa Abu Nujayh, ‘Amr bin ‘Abasa –al-Sulamiyyرضي الله عنه akisema: Nilikuwa nikihisi, enzi za Ujahiliyya [kabla ya Uwislamu] kwamba watu, kwa ujumla, wamepotea; hawafuati haki hata kidogo kwani walikuwa wanaabudu masanamu. (Hadithi ndefu kuhusu kusiliumu kwake Makka hadi kukutana tena na Mtume ﷺ Madina. Anaendelea: )
Basi nikafunga safari kwenda Madina. Nilipofika nikamwendea na kumwambia: “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Unanikumbuka?” Akasema: “Ndiyo! Wewe ndiye yule uliyekutana nami Makka.”
Nikasema:“Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu! Nieleze kile Alichokuelimisha Mwenyezi Mungu na ambacho mimi sikijui! Nielimishe kuhusu Swala.”
Akasema: “Swali swala ya asubuhi, na kisha jizuwiye kuswali mpka baada ya kuchomoza Jua na kuinuka urefu wa mkuki – kwani, wakati huo, huwa linachomoza baina ya pembe mbili za Shetani, na wakati huo ndio makafiri wanalisujudia Jua.
Baada ya hapo, unaweza kuswali, kwani swala wakati huo inatambuliwa na huandikiwa thawabu yule mwenye kuiswali, mpaka kivuli cha mkuki kilingane na urefu wake. Ifikapo wakati huo, jizuwiye kuswali; kwani wakati huo ndio pale Moto wa Jahannam unapokolezwa kuni. Kivuli kikipindukia zaid [ya urefu wa kivuli cha mkuki], unaweza kuswali; kwani swala wakati huo inatambuliwa na huandikiwa thawabu yule mwenye kuiswali hadi kuswali swala ya Asr.
Baada ya Asri, jizuiye kuswali mpaka Jua lichwe, kwani linakuchwa baina ya pembe mbili za Shetani, na wakati huo ndio makafiri wanalisujudia.”
Nikasema: “Ewe Mjumbe wa Mwenyezi Mungu. Nieleze kuhusu udhu.” Akasema:
“Yeyote yule anayejisogezea maji ya kutawadha, akasukutua, na kutema, kisha akapandisha maji puani na kuyatoa, basi kwa kufanya hivyo, makosa yote ya viungo vya uso wake, kinywa chake na pua yake hupukutika na hutoweka, pamoja na maji hayo.
Kisha akiosha uso wake, kama alivyo amrishwa na Mwenyezi Mungu, basi makosa yote ya uso –kwa pande zote mbili za ndevu zake- hupukutika na maji hayo.
Kisha akiosha mikono yake mwili, hadi kwenye vifundo viwili, basi makosa ya mikono yake hupukutika, pamoja na maji, kwenye ncha za vidole vake.
Kisha akipangusa kichwa chake, basi makosa ya kichwa chake hupukutika, na maji, kwenye ncha za nwele zake.
Kisha akiosha miguu yake miwili hadi kwenye vifundo viwili vya miguu, basi makosa ya miguu yake hupukutika, pamoja na maji, kupitia ncha za vidole vyake.
Akisimama akaswali, akamshukuru Mwenyezi Mungu na kumsifu na kumtukuza kama Anavyo stahiki kusifiwa na kutukuzwa, na akaelekeza moyo wake wote kwa Mwenyezi Mungu, basi makosa yake yote hutoweka na kuwa hana makosa kabisa, kama siku aliyozaliwa na mama yake.”
Basi ‘Amr bin ‘Abasa akamsimulia Hadithi hii Abu Umama –swahaba wa Mtume ﷺ . Abu Umama akamwambia ‘Amr: “Ewe ‘Amr! Tahadhari na unayosema! Mtu anapewa malipo yote hayo uliyotaja mahali pamoja!”
‘Amr akamjibu: “Ewe Abu Umama! Mimi nimesha zeeka, mifupa yangu imeshadhoofika, mauti yananisogelea, na sina haja kumsingizia Mwenyezi Mungu wala Mjumbe Wake! Lau ningekuwa sikumsikia Mtume ﷺ akisema maneno hayo, si mara moja, si mara mbili, si mara tatu (akahisabu mpaka saba) basi nisingeliyasimulia kamwe. Lakini, ukweli ni kwamba nimemsikia akisimulia mara nyingi sana.” Ameipokea Muslim. [Angalia pia Hadithi Nan.131]
Amesema Imam Nawawi: Maneno ya Mtume ﷺ : “Baina ya pembe mbili za Shetani.” yaani kuelekea kwenye kichwa chake, na ni mfano wa kumaanisha kuwa wakati huo ndio wakati ambao Shetani na wafuasi wake wanafanya vitimbi vyao vya kufuru na kutaka kuwashirikisha wengine.”
444. Imepokewa kutoka kwa Abu Musa al-Ash’ariyy رضي الله عنه akisema: Amesema Mtume ﷺ
“Akiutakia kheri umma Mwenyezi Mungu, basi humchukua Mtume wao kabla ya wao, na kumfanya awe mtayarishaji wao wa mambo mazuri, na pia hazina yao Siku ya Kiyama.
Na akiutakia shari umma basi huuangamiza vile Mtume wao yungali hai; akiona kwa macho yake jinsi wanavyo angamizwa. Na huko ni kumliwaza kwa walivyo mkadhibisha na kukataa kufuata maamrisho yake kwao.” Ameipokea Muslim.
UFAFANUZI.
Hadithi hizi mbili na Aya iliyotangulia, zinatuhitimishia maudhui ya mlango huu, ya kuwa na matumaini mema na Mwenyezi Mungu. Kwani Kutawadha udhu kamilifu, na kuswali rakaa mbili kwa utulivu na – sunna ya baada ya kutawadha- kunatosha kuwa ndio sababu ya kufutiwa dhambi zote –isipokuwa dhambi kubwa kubwa الكبائر .
Na itoshe, kwetu sisi, kushukuru kwamba Umma huu, ambao sisi tumo, tumerehemewa na Mwenyezi Mungu سبحانه وتعالى kwa kumchukua Mtume Wake na kutuacha sisi tumfuatie mmoja mmoja, ili atutangulie mbele ya Mwenyezi Mungu. Hiyo, peke yake, inatosha kutupa matumaini makubwa kwa Mola wetu.
YALIYOMO NA YATOKANAYO.
1. Fadhila za Udhu na fadhila za rakaa mbili za sunna ya Udhu.
2. Umuhimu wa kutawadha kikamilifu na kuswali kwa unyenyekevu.
3. Inakatazwa kuswali baada ya Swala ya Alfajiri, wakati wa kuchomoza Jua, hadi liinuke kadiri ya urefu wa mkuki.
4. Inakatazwa kuswali baada ya Swala ya Laasiri na wakati Jua linakuchwa.
5. Nyakati hizi mbili ni vibaya –yaani makuruhu- kuswali swala yoyote, pasi na dharura.
6. Fadhila za Kuswali Swala ya Dhuha, na wakati wake ni tokea baada ya Jua kuinuka urefu wa mkuki, hadi majira ya Swala ya Adhuhuri –i.e. kivuli cha urefu wa mkuki kuwa sawa na urefu wa mkuki weneywe, upande wa magharibi-.
7. Fadhila za Sunna baada ya Adhuhuri na kabla ya kuswali Swala ya Laasiri. Kwani wakati huo, hata malaika huswali pamoja, na kushuhudia Sunna zako.
8. Wajibu na Umuhimu wa unyenyekevu katika Ibada.
9. Ukosefu wa unyenyekevu, katika ibada, unapunguza thawabu za ibada hiyo.
10. Fadhila na Umuhimu wa Mwislamu kuwa na matumaini mema na Mwenyezi Mungu.
11. Kuwa na matumaini na Mwenyezi Mungu ni kutenda mema na SI kubweteka.
12. Kubweteka na kujipa matumaini kwa Mwenyezi Mungu ni kujidanganya.
13. Kutawakali ni kumuamini Mwenyezi Mungu na kutenda ya aliyokuamrisha kuyatenda.
14. Fadhila za Abu Nujayhi رضي الله عنه
15. Uangavu, umakini na ukali wa ubongo wa Mtume ﷺ kumtambua mtu, aliyekutana naye, zaidi ya miaka 10 iliyopita!
16. Hima, hekima na busara ya Mtume ﷺ katika kuongoza na kuelimisha Maswahaba wake.
17. Umma wa Muhammad ﷺ umebahatika kwa kutopatilizwa, kabla ya yeye kuitikia Wito wa Mola wake.
18. Kutangulia kwa Mtume, yeyote yule, kwenda kwa Mola wake ni rehema kwa Umma wake.
19. Watu walioangamizwa kabla ya vifo vya Mitume wao, wamelaaniwa na kutengwa na Rehema za Mwenyezi Mungu.
20. Hatari ya kwenda kinyume na mafundisho na mafunzo ya Mtume Muhammad ’ﷺ ; kwani hakuna usalama kwa kufanya hivyo.
21. Uokofu ni kufuata aliyokuja nayo Bwana wetu, Muhammad ﷺ , tu.
والله أعلم
وبالله التوفيق
السيد عبد القادر شريف آل الشيخ أبى بكر بن سالم.
Imetayarishwa na Sayyid Abdulqadir Shareef
Kutoka Kitabu cha: Kitalu cha Waja Wema: Maneno ya Muokozi wa Umma, ambacho ni tafsiri kamili ya رياض الصالحين من كلام سيد المرسلين للإ مام النووي kilicho tungwa na Imam An-Nawawi na kufasiriwa kwa Kiswahili na Sayyid Abdulqadir Shareef Aal Shaykh Abi Bakr bin Salim آل الشيخ ابى بكر بن سالم.
NI RUHUSA KUNUKUU, kama ilivyo, pasi na kubadilisha au kuongeza, na kuweka kwenye FB yako au kwenye WhatsApp na kwenye Makundi ya Mitandao ya Kijamii za Kiislamu, kwa lengo la kusambaza na kuelimisha Dini. Changia kusambaza Dini, ujipatie thawabu.
kcwajawema@gmail.com